Ikisiri
Bwana Yesu asifiwe
ni miongoni mwa semo ambazo hutumiwa mara kwa mara na baadhi ya waumini wa makanisa ya Kikristo. Licha ya usemi huo kuwa na maana yake ya msingi, hutumiwa kwa dhima mbalimbali za kipragmatiki. Makala hii inalenga kuchunguza dhima hizo ili kuongeza maarifa kuhusu namna muktadha unavyochangia kupata maana katika lugha. Matokeo kutoka katika sharika tatu za Kanisa la Kilutheri yanaonesha kwamba usemi
Bwana Yesu asifiwe
una dhima mbalimbali, zikiwamo kusalimia, kuanzisha mazungumzo, kuziba pengo la ukimya, kusisitiza jambo na kuchangamsha waumini. Kwa kuzingatia matokeo haya, makala hii inahitimisha kwamba dhima za usemi
Bwana Yesu asifiwe
zinaweza kueleweka vizuri pale msikilizaji anapohusisha muktadha wa kiutamaduni, kipragmatiki na kilongo husika.