Suala la uana limetafitiwa na watafiti mbalimbali katika jamii za Kiafrika na ulimwengu kwa jumla. Lugha na uana ni masuala mawili ambayo hayatengani. Wanajamii mbalimbali wanapozungumzia uana ambao ni ugavi wa majukumu baina ya wanawake na wanaume, wanatumia lugha kuwasilisha ujumbe huo. Lugha inayotumiwa na wanajamii kurejelea wanawake na wanaume huwa ni ya kimafumbo, hasa methali, misemo, vitendawili na nahau. Semi zingine za misemo na methali zinazosawiri uana, zinawarejelea wanaume na wanawake kichanya na kihasi mtawalia. Makala haya yalijikita katika madhumuni ya pili ya tasnifu ya uzamili iliyohusu uchanganuzi wa maana kijamii za semi zinazosawiri uana katika lugha ya Kiswahili. Mtafiti wa makala haya aliongozwa na nadharia ya Uwezo- uume na nadharia ya maana kijamii. Nadharia ya Uwezo uume iliasisiwa na (Robert Bly, 1991) na kuendelezwa na (Connell, 1995). Kulingana na waasisi hawa, nadharia hii hubainisha nguvu na mamlaka yanayomilikiwa wanaume, hasa kutokana na utamaduni wa jamii husika. Nadharia ya Maana kijamii iliyoasisiwa na Lev Vygotsky (1978) inaeleza kwamba, maana kijamii inatokana na muktadha unaotawaliwa na elementi za kijamii kwa mfano lahaja, imani na tamaduni za kijamii. Maana kijamii ya kila methali na misemo inayosawiri majukumu ya uana mathalani ubabedume, kazi, malezi, ukware, ndoa, urembo, mapenzi ya pesa na uwezo wa akili, ilichanganuliwa katika makala haya. Mtafiti wa makala haya alitumia muundo wa kimaelezo. Utafiti huu ulikuwa wa nyanjani na maktabani. Mtafiti alitumia sampuli ya uchunguzi wa sensa na kolevu. Mbinu ya majadiliano na kundi lingani na usomaji wa nyaraka za kimaandishi zilitumiwa kukusanya data. Data zilichanganuliwa kimaelezo kutegemea madhumuni ya utafiti. Matokeo ya utafiti huu yalibaini kwamba, maana kijamii za methali nyingi zinazosawiri uana, zinaegemea wanawake kwa upande wa uhasi na wanaume kichanya